• Instagram
  • Twitter
  • Facebook
  • Google+
  • RSS Feed

Thursday, March 17, 2016

Daraja la Kigamboni Kuanza Rasmi Aprili 16

No comments:
 

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mh. Profesa Makame Mbarawa

Serikali imesema imesema daraja la Kigamboni lenye urefu wa mita 640 litafunguliwa rasmi, Aprili 16, mwaka huu.

Daraja hilo, linajengwa kwa ushirikiano kati ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) na serikali kwa gharama ya dola za Marekani milioni 143.5 (Sh. bilioni 216), ulipangwa kumalizika ndani ya miezi 36 tangu kuzinduliwa kwake Septemba, 2012.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, aliyasema hayo jana kupitia taarifa iliyotolewa na kitengo cha mawasiliano serikalini cha wizara hiyo.

Mbarawa alisema kazi inayoendelea sasa ni kupitisha magari maalum kwa ajili ya kupima ubora wa daraja ili kujiridhisha kabla ya kukabidhiwa rasmi serikalini.

Januari 27, mwaka huu, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mhandisi Joseph Nyamhanga, aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akisema daraja hilo lingeanza kutumika Machi Mosi, mwaka huu.

Mbarawa amewataka watumiaji wa daraja hilo kuwa waangalifu, kulinda miundombinu na kuepuka vitendo vya hujuma ili lidumu kwa muda mrefu.

Daraja la Kigamboni likiendelea katika ujenzi. Linatoka Kurasini hadi Kigamboni. Lina urefu wa mita 640

“Daraja hili lina urefu wa mita 640, barabara sita, tatu zinapanda na tatu zinashuka, hivyo tunawaomba wananchi watakaovuka kuzingatia usafi na ustaarabu,” alisema Mbarawa.

Waziri Mbarawa alisema serikali pia itaweka sheria kali kwa wote watakaokiuka matumizi sahihi ya daraja hilo na kusisitiza umuhimu wa madereva kuzingatia sheria za usalama barabarani wanapovuka katika daraja hilo.

Naye Meneja Msimamizi wa Ujenzi wa daraja hilo, Karim Mattaka, alisema wataalamu wanaendelea na taratibu ili kujiridhisha kama linamudu kupitisha uzito uliokusudiwa, kabla ya kulikabidhi kwa serikali.

Alisema awamu ya kwanza ya kulipima daraja hilo imekamilika na sasa wanaendelea na awamu ya pili hadi watakapomaliza awamu nne ili kujiridhisha kabla ya kuanza kutumika.

Wakati huohuo, Waziri Mbarawa amemteua Profesa Ninatubu Lema kuwa mwenyekiti wa Bodi ya Usajiliwa Wahandisi (ERB) kwa kipindi cha miaka mitatu hadi Machi 10, 2019.

Pia amewateua Profesa Esnat Chaggu, Mhandisi John Ngowi, Mhandisi Gema Modu, Mhandisi Othman Khatib, Mhandisi Nuberis Nyange, Mhandisi Paul Basondole, Mkadiriaji Majenzi Samweli Marwa na Evelyn Marwa kuwa wajumbe wa ERB.

No comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...
 
© ALLSTARTZ.BLOGSPOT.COM 2012 - 2017 | ALL RIGHTS RESERVED | CODE + DESIGN BY: DMZ