• Instagram
  • Twitter
  • Facebook
  • Google+
  • RSS Feed

Thursday, January 7, 2016

BIASHARA HUANZA NA WAZO,BAADA YA WAZO KUNA NJIA ZA KUFUATA ILI BIASHARA YAKO ITAMBULIKE KISHERIA KAMA IFUATAVYO

No comments:
 
Biashara huanza na wazo linalotokana na ndoto au shauku. Mathalani vijana wengi wanapenda kuwa na vitu vya


 thamani kama magari ambavyo kwa mshahara hawawezi kuvipata. Kama una ndoto ya kuwa na vitu vya 

thamani sharti ufikirie kuanzisha biashara ili kuongeza mapato. Wazo la biashara huzaa ubunifu ambao hufanya

 biashara unayotaka itokee.Ukiwa na wazo la biashara basi tafuta taarifa zitakazokuwezesha kufanya maamuzi

 sahihi. Ni vizuri wazo liwe ndani ya kitu unachokipenda na unakiweza. 


Baadhi ya taarifa muhimu ambazo unapaswa kuzitafuta ni, je biashara unayoifikiria inahitajika? Uhitaji wa

 huduma/bidhaa unagusa kundi gani la watu? Kundi hilo linaguswa kwa kiasi gani? Gharama za kuanzisha

 biashara? Je mahitaji ya wateja yatatatulika? Na je walengwa wana uwezo wa kulipia? Taarifa hizi unaweza 

kuzipata kwa kuuliza wanaofanya biashara kama hiyo, kuangalia hali halisi, kusoma maandiko, kupata ushauri

 wa kitaalam, na vyanzo vingine. Mbinu nyingine ambazo unaweza kuzitumia kupata wazo la zuri la biashara ni 

kwa kujiunga vilabu au vikundi vya kimaendeleo, kuhudhuria semina na mikutano. MTAJI WA KUANZIA

 BIASHARA Kuanza biashara kunahitaji mtaji kulingana na aina na kiwango cha biashara unachotaka kuanzia.

 Mtaji huo utatumika katika mambo mengi yakiwemo kuanzisha biashara yenyewe, kulipia pango na usajili. 

Hata hivyo mtaji hutoka katika vyanzo vingi lakini chanzo muhimu ni akiba binafsi au kukopa kutoka kwa ndugu

 au familia au mkopo. Hata hivyo inashauriwa usitumie mkopo wa benki kuanzishia biashara bali tumia mkopo

 kuendeleza biashara. Hivyo basi ni vizuri kwa anayetaka kuingia kwenye ujasiriamali kuanza kujiwekea akiba. 

Njia ni nyingi mno za kupata mtaji. ENEO LA BIASHARA Baada ya kuhusu wazo lako la biashara sasa ni wakati

 wa kutafuta eneo la biashara ambalo lazima liwe ni rahisi kumwelekeza mtu, linafikika kiurahisi, kuna 

mwingiliano wa watu, na kuwa na uwezekano wa kubandika bango la biashara yako. KUANDIKISHA BIASHARA 

Kabla ya kuanza biashara, sharti isajiliwe kwa mujibu wa sheria za nchi. Jina la Biashara Biashara sharti iwe na 

jina na inaweza kuandikishwa kama ya mtu mmoja, kampuni, ushirika au ubia. Kama biashara yako itakuwa ya 

mtu mmoja (sole proprietorship) itakupasa kufuata utaratibu huu:-

(1) Chagua jina la biashara 

(2) Andika barua kwa Mkurugenzi wa BRELA ukiomba kuangaliziwa jina ulilochagua kama halijasajili na mwingine (kwa sasa unaweza kuangalia mwenyewe kutoka tovuti: www.brela-tz.org),

(3) Baada ya jina kupita jaza fomu nambari 2 na 3 ambazo unaweza kuzipata toka tovuti ya BRELA

(4) Lipia ada ya usajili ya Sh. 6,000/= 

(5) wasilisha fomu na baada ya siku chache utapatiwa hati ya usajili. 

Kama unataka kusajili kampuni yenye ukomo (Limited Liability) itakulazimu kuzingatia yafuatayo:- 

(1) Kampuni lazima iwe na watu si chini ya 2 na wasizidi 50 

(2) hakikisha jina la kampuni utakalopendekeza liwe halijawahi kutumika katika tovuti ya BRELA: www.brela-tz.org 

(3) Andaa hati ya makubaliano (MEMARTs)

(4) Jaza fomu nambari 14a na 14b

(5) Hakikisha MEMARTs na fomu 14b zimesainiwa na wakili au mwanasheria

(6) Lipia gharama za usajili kulingana na mtaji unaoanza nao, 

(7) Wasilisha maombi yako na hati ya usajili itatolewa baada ya muda mfupi. 

JISAJILI KAMA MLIPA KODI (TIN NUMBER) Mfanyabiashara pia anapaswa kujisajili mamlaka ya kodi – TRA. Ili kujisajili unapaswa kuzingatia yafuatayo:-

(1) uwe na hati ya usajili

(2) uthibitisho wa eneo la biashara. LESENI YA BIASHARA

 Biashara zote lazima ziwe na leseni na vibali maalum ambazo hutolewa na ofisi za biashara za halmashauri ya

 Manispaa au Wilaya ya eneo la biashara yako. Baada ya kupata leseni na vibali toka maamlaka husika 

unaweza sasa kuanza biashara yako.




No comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...
 
© ALLSTARTZ.BLOGSPOT.COM 2012 - 2017 | ALL RIGHTS RESERVED | CODE + DESIGN BY: DMZ